Friday, 6 January 2017

MAHUBIRI YA JUMAPILI YA UBATIZO WA BWANA WETU YESU KRISTU


1. Isa42: 1-4,6-7
2. Mdo 10:34-38
Injili: Mt 3:13-17

"  Daima tufanywe viumbe wapya katika Kristo kwa njia ya ubatizo wetu"


Kuna kisa cha mtu mmoja aliyeenda kwa muuza nguo na mshona nguo, aliingia mahali pale na kuangaza kuzunguka katika hilo duka la muuza nguo kwa kuangalia mavazi mbalimbali yaliyokuwemo mle dukani, na baadaye huyo mtu ambaye umri wake kidogo ulikuwa ni umri wa uzee alirudi kwa huyo muuza nguo na kumwambia, tafadhali naomba unitengezee vazi zuri la kike namna ya mkaja lakini lisiwe kubwa liwe dogo kiasi, maana kesho ni siku ya mjukuu wangu. Huyo mtu aliendelea kubainisha kuwa lile vazi lilikuwa kwa ajili ya mjukuu wake.


Mtengeneza nguo alipata kuwa na shahuku ya kujua umri wa huyo aliyekuwa akiombewa na Babu yake atengenezewe hiyo nguo maalum, " mjukuu wako ana miaka mingapi?", mzee alijibu," hadi sasa ninapoongea hii ni siku ya saba tangia azaliwe" mtengeneza nguo alibaki ameduwaa kwa kuwa hilo lilikuwa siyo jambo la kawaida. Hivyo huyo mzee aliendelea kusisitiza hilo vazi litengenezwe vizuri kwa kusema, " hakikisha hilo vazi linapendeza, maan kesho ni siku ambapo mjukuu wangu ni siku yake yakukutana na Mungu" kwa mshangao yule muuza nguo aliendelea kuwa na wasiwasi, kwa kumuuliza tena yule mzee kwa mshangao," kukutana na na Mungu?? mzee alijibu, " kesho ni siku yake ya kubatizwa"


Wengi wetu hata kama siyo wote tulibatizwa tukiwa bado wadogo sana kiasi kwamba saa nyingine huwa inatuwia vigumu kukumbuka ile siku muhimu katika maisha yetu ambapo tulibatizwa na tukawa wana wa Mungu. Hatuwezi kukumbuka na kujua ni namna gani siku ya ubatizo wetu wazazi wetu, wazazi wetu wa ubatizo walivyokuwa wanajibu maswali na kukiri imani kwa niaba yetu?? Huu ndoo wakati ambapo tulipata majina yetu kwa njia ya ubatizo.


Leo ni siku ambayo tunafanya sherehe ya ubatizo wa Bwana wetu Yesu Kristu, twaweza jiuliza maswali mengi sana juu ya kwanini Yesu alipata kubatizwa kule mto Yordani?  Sakramenti ya ubatizo maana yake huwa ni kuondoa dhambi ya asili, hivyo twaweza jiuliza kuwa hivi Yesu alibatizwa kwa kuwa alikuwa na dhambi ya asili pia? Jibu ni kwamba hakuwa na hiyo dhambi ya asili, na kwa kubainisha hilo mtakatifu Ambrozi mwalimu wa Kanisa alikuwa na haya ya kusema juu ya ubatizo wa Bwana wetu Yesu Kristu:  " Bwana wetu Yesu Kristu alibatizwa si kwa sababu ya dhambi ya asili, bali alibatizwa ili akayasafishe na kuyatakasa maji ili yawe
na nguvu ya ubatizo" 


Ni kwa msingi huo tunaona Kristu anabatizwa ili apate kuunganika na sisi katika ubinadamu wetu uliodhaifu hasa akiungana nasi katika ile safari yetu ya hija ya ufalme wa mbinguni. Hivyo yupo nasi na ni mmoja wetu. Kila mmoja wetu atambue amezaliwa na dhambi ya asili, Kanisa ni chombo cha Mungu ambapo hiyo dhambi ya asili huondolewa na hivyo sisi kuitwa watoto wa Mungu. Naye mtakatifu Vincent Ferrer alikuwa na haya ya kusema juu ya ubatizo; " kila mkristu mbatizwa inabidi atambue kuwa ni ndani ya tumbo la Kanisa kila mmoja wetu hugeuzwa kutoka kuwa mwana wa Adamu kuwa mwana wa Mungu."dhambi ya adamu iliyofanya wote tukawa na dhambi ya asili, hiyo dhambi ya asili huondolewa na nguvu ya sakramenti ya ubatizo na hivyo kutufanya tusiwe chini ya uvuli wa Adamu, bali tuwe viumbe wapya katika Kristu.


Ubatizo kwetu maana yake ninini?ubatizo ni sakramenti tuipokeayo, ambayo hutuosha dhambi ya asili na hatimaye sisi huitwa wana wa Mungu. Daima ili tuwe wana wa Mungu ni lazima sote tushiriki ule ubatizo wa Bwana wetu Yesu Kristu. Kristu anavyobatizwa ni kiashilio cha kuanza kwa utume wake, ni kiashilio cha kutangaza ufalme wa mbinguni hapa duniani, wengine waliozoea lugha ya wanasiasa utasikia hapa na pale wanasema neno, ' sela' na vivyo hivyo kwa ubatizo Kristu mwenyewe anajiweka wakfu kwa ajili ya kazi aliyotumwa kufanya duniani, na kazi kubwa kuliko zote ilikuwa ni kuutangaza ufalme wa Mungu kwa mataifa na vizazi vyote.


Kwa njia ya ubatizo tunazaliwa upya kwa maji na Roho Mtakatifu. Tunakuwa tumetakaswa kutoka dhambi ya asili na hivyo tunakuwa wana wa Mungu. Kwa njia ya ubatizo huwa ndo tunaingizwa Kanisani na kuwa moja ya jamii ya wakristu wanaounda kanisa duniani. Hii hatua ya kuingizwa kanisani kwa waliobatizwa yaweza fananishwa na moja ya mila zetu ambapo mmojawapo akitaka kuhesabiwa kuwa ni mmoja wa wanaukoo fulani katika jamii husika, hupitia hatua iitwayo jando( initiation- rites of passages) sasa nasi wakatoliki tuko sambamba na lile lifanyikalo katika tamaduni zetu, sisi jando yetu huwa ni kumwandaa mtoto/mkatekumeni kwa hatua ili aweze kupokelewa kanisani na hatimaye kuwa mwanajumuiya kamili wa kanisa linaloungama imani moja.

Sakramenti ya ubatizo ni alama na ishara inayotukumbusha kuwa tumejiweka wakfu katika ufalme wa Mungu. Kupitia ubatizo ni dhahiri kuwa huwa tunakuwa tayari kumtumikia Mungu kama manabii, wafalme, na makuhani. Kwa njia ya sakramenti ya ubatizo huwa tunaimarishwa pia na roho mtakatifu, kwani ile siku ambayo kila mmoja wetu hubatizwa humpokea roho mtakatifu pia. Huyo roho mtakatifu tumpokeaye wakati wa ubatizo ni yule roho ambaye hutupa nguvu za kupambana na vishawishi na pia kupambana na magumu mbalimbali.

Juu ya nguvu ya Sakaramenti ya ubatizo Papa Benedict xvi alikuwa na haya ya kusema, " thamani ya ubatizo  ni msingi imara wa umissionari kwa kila mmoja wetu aliyebatizwa, kwa kuwa yule ambaye amependa kumshuhudia Kristo Yesu kwa njia ya ubatizo ni lazima afuate nyayo zake yule aliyemshuhudia kwa njia ya matendo. Hivyo kwa njia ya ubatizo tumekuwa warithi katika kufanya kazi ya Bwana kwa njia ya umissionari."


Kwa kumalizia hebu tuangalie zile sifa kuu za Kristu aliyebatizwa, je naweza kulinganisha hizo sifa za Yesu mbatizwa na maisha yangu?
Yesu alikuwa maskini lakini mimi siyo maskini.
Yesu alikuwa mnyenyekevu na mtii, lakini mimi siyo mtii.
Yesu alikuwa mpole, lakini mimi siyo mpole.
Yesu alisamehe, lakini mimi naweka roho ya kulipiza visasi.
Yesu alitii mamlaka, lakini mimi daima hutaka kutotii na saa nyingine kuwaamlisha wengine kwa faida yangu.
Yesu alichukiwa kwa sababu ya ukweli, mimi nauzika ukweli ili nipendwe zaidi na nilinde maslahi yangu.
Yesu alipaa mbinguni kwa njia ya mateso na msalaba, lakini mimi kwa upande wangu nataka kufika huko kwa njia ya starehe na raha bila ya msalaba.

Je hiyo ni sawa kuwa mtumishi awe hivyo kuliko yule mwalimu wake?

No comments:

Post a Comment