Thursday, 5 January 2017

MAHUBIRI YA JUMAPILI YA EPIFANIA MWAKA A


1. Isa.60: 1-6
2.Ef 3:2-3,5-6
Injili: Mt 2:1-12

"  Hata asili yaweza kuongea na kumpeleka mtu kwa Mungu"

Ndugu zangu basi niwaalike tuweze kutafakari Neno la Mungu pindi tunapoadhimisha Jumapili ya tokeo la Bwana wetu Yesu Kristu yaani, Epifania.

Katika masomo yetu hasa somo la injili twaweza baini kuwa katika safari yetu ya imani kuna aina tatu za watu; wale ambao humtafuta Mungu na kumtumikia; wale ambao wanamtafuta Mungu lakini bado hawajamwona; na mwisho wale ambao hawana haja/shauku ya kumtafuta Mungu. Kundi la kwanza la aina ya watu wamtafutao Mungu ni lile kundi la watu wenye amani na furaha, kundi la pili ni lile kundi la watu wenye uso wa huzuni kwa sababu wanamtafuta Mungu lakini hawajamwona katika maisha yao, nalo kundi la tatu ni kundi la wajinga, yaani wale ambao hawana hata hamu ya kukutana na Mungu mwumba wao.

Tunaona hizo aina tatu za wale wamtafutao Mungu kama inavyodhihirishwa katika masomo yetu, hebu tuone aina mojawapo, ambayo hii ni aina ya tatu ya wale wamtafutao Mungu, yaani kundi la wajinga ambao hawa daima hujifanya wanamtafuta Mungu kumbe ndani yake wana hila ya kufanya maovu kwa kutumia hiyo nafasi. Basi ni kwa msingi huu twaweza sema kuwa aina hii ya tatu kadiri ya somo la injili inaangukia kwa mfalme Herode, huyu anajifanya kumtafuta Mungu kumbe anazo hila nyingi ndani yake, yeye lengo lake ilikuwa kutafuta kumwua Yesu ili apate kulinda madaraka yake yasipokonywe na huyo mfalme aliyezaliwa. Tunaambiwa kuwa mfalme Herode kwa kusutwa na dhamila yake mbaya anaamua kuwa ua hata watu wa familia yake akiwemo mke wake Mariamme na watoto wake wawili. Herode kimsingi anawakilisha kundi la watu ambao hutumia madaraka vibaya, watu ambao hujifanya wako karibu na Mungu kumbe wana malengo mengine.

Pia tunaona kundi jingine la wale wamtafutao Mungu na kukutana naye na hatimaye kumtumikia, basi hili siyo kundi jingine bali ni Yosefu na Maria, na pia katika hilo kundi twaweza kujumuisha wale wachungaji( Lk2:8-12). Hivyo ni kwa msingi huu twaweza sema kuwa hili ni kundi lenye amani na furaha kwa kuwa wamekumkutana na Mungu.


Kundi jingine la watu wamtafutao Mungu, ni Mamajusi, hawa ni wale wamtafutao Mungu kwa nguvu zao zote na juhudi zao zote bila ya kuchoka. Mamajusi ni neno ambalo lina msingi wake kutoka lugha ya Kigiriki " Magoi" ambapo nalo hilo limezaa neno la kiingereza, " magic" au " magician" hawa mamajusi walikuwa siyo wachawi kama tuwaonao kwenye mazingira yetu, bali hawa walikuwa ni wataalamu wa nyota, na hivyo katika ufumbuzi wao walikuwa wakitaka kujua uhusiano uliopo kati ya nyota na dunia. Hawa kwa ujuzi na utaalamu wao waliitwa watu wa hekima kwa kuwa wao walifuata alama za asili na hizo alama za asili ziliwaongoza hadi kwa Kristu.


Kwa upande wetu ni nyota ipi ambayo inaweza tupeleka kwa Kristu? Je mimi ni nyota ya kumpeleka mwingine kwa Kristu? Ni nyota ipi ya kwanza ambayo ilikupeleka wewe kwa Kristu Yesu?? Jibu ni kwamba ile nyota ya kwanza ambayo ilinipeleka mimi na ikakupeleka kwa Kristu Yesu ni wazazi wetu/ walezi wetu pindi tulivyokuwa wadogo au tukishakuwa watu wazima, tukiikumbuka ile siku yetu ya kwanza tulipobatizwa na kuitwa wana wa Mungu katika Yesu Kristu mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote. Wazazi wetu/ au walezi wetu, au malezi mazuri ya Kikristu na elimu ya maandiko matakatifu, walimu na watu wenye maarifa mbalimbali, kwa msingi huo twaweza sema kuwa,  hizo zote ni nyota ambazo zimetupeleka kwa Kristu na hizo ndoo nyota ambazo zinatuongoza hadi kwa Kristu hadi leo hii.


Mamajusi walimpelekea Yesu dhahabu, uvumba, na manemane,zikiwa ni alama za mali asili za dunia. Hata hivyo kwa upande wetu sisi hatuna haja ya kumpelekea Mungu dhahabu, manemane, na uvumba, baadala yake sisi Yesu tunampelekea Mioyo yetu, akili zetu na utashi wetu wa kumtumikia na kukaa naye daima, hizo kimsingi ndoo zawadi zetu kubwa kwa Yesu Kristu. Dhahabu, uvumba na manemane vyaonekana kuwa vilikuwa ni vitu vya thamani sasa kwa wakati ule hata hadi nyakati zetu.


Hawa mamajusi kwa kubeba hivyo vitu na kumpelekea Kristu ni fundisho kwetu kuwa hawa, wanatupa ishara ya kuacha mali dunia, kuacha mambo mengi ya dunia yenye thamani na kisha kumtafuta Kristu na hatimaye kuweza kukaa naye. Sisi upande wetu nasi twaweza labda jiuliza swali moja kubwa kuwa ni vingapi tulivyo navyo kama vile utajiri, hela na mali nyinginezo zinatuzuia kwenda kwa Kristu? hawa mamajusi wametumia huo utajiri ili uweze kuwafikisha kwa Kristu.


Kumbe kwetu nasi hili liwe somo na fundisho kuwa vile vyote tulivyonavyo kama mali, utajiri na vingine vingi, basi kumbe twaweza vitumia kama njia ya kutufikisha kwa Yesu Kristu. Mfano kama unamiliki gari, basi hilo gari litumie liwasaidie watu baadala ya kuleta matatizo, kama una miliki simu ya kisasa, tumia hiyo nafasi ya kumiliki hiyo simu katika kuinjilisha na kumtangaza Kristu baadala ya kutumia hiyo simu kutenda maovu, kama una akili nyingi, basi itumie hiyo akili uwasaidie watu wapate kumfikia Kristu kwa urahisi, kama wewe ni daktari basi tumia hicho kipaji cha utabibu ili uwape watu maisha baadala ya kuwaondolea maisha, kama wewe ni mwalimu, basi wafundishe watu mambo mazuri na njia njema za kufika kwa Kristu, na kama wewe ni padre, askofu, mchungaji, basi tumia hiyo kalama yako ya huo uchungaji ili uwavute watu kwa Kristu Yesu.  Ni kwa msingi huo mimi naweza sema kuwa pia ni mamajusi na wewe ni mamajusi wa kupeleka tulichonacho kwa Kristu na kubaki naye daima.


Nimalizie tafakari hii kwa kisa hiki: Kulikuwa na mtu mmoja ambaye alifanya kazi katika kiwanda cha pamba, huyu alikuwa ni mkristu aliyejiwekea utaratibu wa kutokula nyama siku za ijumaa akiendelea kutafakari mateso ya Kristu msalabani. Huyu daima siku za ijumaa alibeba mayai na samaki kidogo kwa ajili ya mlo wake pindi awapo kazini. Hivyo wafanyakazi wenzake ambao walikuwa siyo wakatoliki walimtania na kumbatiza jina la " Bwana mayai na masamaki" wakati wao siku zote walikuwa wakila wali kwa nyama. Na mbali ya kutaniwa na kufanyiwa kejeli za namna hiyo, huyo ndugu hakuacha ule utaratibu wake wa kubeba hicho kitoweo chake siku za ijumaa.


Huyo mtu miaka baadaye alipata kukutana na mtu mmoja ambaye alikuwa amevalia mavazi ya upadre akitokea Kanisani, hao wawili walipata kutambuana na hivyo kupata kuhabarishana mambo mengi sana.


Hapo baadaye  huyo padre aliyekuwa akitoka mlango wa Kanisa alimwambia yule ndugu: " Ilikuwa ni mfano wako mzuri ndoo ulinifanya niingie ukatoliki. Nilikumbuka zile siku ambazo ulikuwa unabeba samaki na mayai kazini kwako na pia ukaanza kudhalauliwa na kuchekwa na ndugu zako uliofanya nao kazi, lakini na mbali ya hayo madharau hukuacha/ kuikana imani yako, na umedumu kwa kuilinda imani yako, nami kwa kuona hivyo nikaamua kujiunga na ukatoliki maana nilifikiri sana kuwa kama huyu amedharauliwa namna hiyo na akazidi kuishi na kuilinda imani yake, vivyo ni lazima kutakuwa na kitu cha pekee kwa wakatoliki. Ni kwa jinsi hiyo niliamua kufuata imani ya Kanisa Katoliki. Leo nimeadhimisha misa yangu ya kwanza ya Shukurani." huyo padre alimalizia kutoa ushuhuda wake kwa huyo ndugu.


Epifania maana yake ni kumdhihirisha Kristu, kumfunua Kristu kwa wale ambao bado hawajapata kutambua uwepo wake katika maisha yao. Kwa kuwainjilisha watu kwa mifano bora hasa kupitia maisha yetu tunavyoishi, ni dhahiri kuwa sisi tunakuwa ni nyota za kuwapeleka watu kwa Kristu.


Tutabaki kujiuliza hili swali kuwa je mimi ni nyota ya kuwapeleka watu kwa Kristu? Je kama ni nyota nimewapeleka wangapi kwa Kristu? Daima tuwe nyota zenye mwanga wa kuwapeleka watu kwa Kristu.



No comments:

Post a Comment