Wednesday, 11 January 2017

MAHUBIRI JUMAPILI YA PILI YA MWAKA A


Isa 49:3; 5-6
2.1Kor 1:1-3
Injili:1:29-34

                    " Je na wewe ni mwanakondoo?"

Wapendwa familia ya Mungu tunaposheherekea jumapili ya pili ya kipindi cha kawaida cha mwaka wa Kanisa tunaalikwa kutafakari juu ya Yesu kama mwanakondoo wa Mungu. Wazo kuu ambalo litatuongoza katika tafakari yetu ni juu ya huyo mwanakondoo wa Mungu kwetu ana maana gani na je twaweza kujifunza nini kutoka kwake huyo mwana kondoo wa Mungu.

Katika Injili tunamsikia mwinjili Yohane akigusia hili jambo kwa ukaribu, katika Injili Yohane anasema, " tazama mwanakondoo wa Mungu aondoaye dhambi za dunia"( Yohane1:29). Katika mazingira ya kawaida na uelewa wetu wa kawaida pindi tusikiapo neno, " Mwanakondoo"  picha ambayo hutujia akilini mwetu ni juu ya yule mtu ambaye ni mpole sana, mnyenyekevu, au yule ambaye hana sauti katika jamii. Lakini hata hivyo tunapata motisha hapa kuwa Yesu alikuwa hana hiyo picha ya mwanakondoo kama wengi ambavyo tunaweza fikiria. Baadala yake Yesu ni mwanakondoo ambaye amepewa sifa ya kuondoa dhambi za dunia, hivyo huyo ni mwanakondoo mwenye nguvu, ni mwanakondoo hasiye dhaifu, ni mwanakondoo ambaye yupo tayari kuufia ukweli. Huyu ni mwanakondoo ambaye yupo tayari kubeba  hata lawama ili atimize mapenzi ya Mungu.

Kutoka katika maandiko matakatifu twaweza pata picha mbili juu ya huyo mwanakondoo. Kwanza kabisa ni kuwa huyo mwanakondoo damu yake inamwagika kwa ajili ya wengine. Hii taswira ya huyo mwanakondoo ambayo mwinjili Yohane anatufundisha katika injili inapata mizizi yake kutoka moja ya vitabu vya agano la kale. " Nao watatwaa baadhi ya damu yake na kuitia katika miimo miwili na katika kizingiti cha juu katika zile nyumba watakazomla."( Kut12:7) "

Kwa kuwa Bwana atapita ili awapige hao wamisri; na hapo atakapoiona hiyo damu katika kizingiti cha juu, na katika ile miimo miwili, Bwana atapita juu ya mlango, wala hatamwacha mwenye kuharibu aingie nyumbani mwenu."( Kut 12: 23). Ni kwa msingi huo tunapata ufahamu na uelewa juu ya hii taswira ya Yesu kama mwanakondoo kuwa Yeye ajitoa sadaka kwa ajili ya wengine. Ni kwa msingi huu twaweza sema juu ya utumishi, kuwa yeyote ambaye anataka kuwa kiongozi lazima auvae ule utu wa Kristu kama mwanakondoo. Yeyote ambaye ni kiongozi kwa maana ya kuwatumikia watu, huyo hana budi kuitwa mwanakondoo. Kuwa kiongozi katika hii taswira/picha ya mwanakondoo ni kukubali kukabiliana na hali zote yakiwemo magumu katika kumfuasa Kristu mwanakondoo wa Mungu. 


Mateso katika maisha yetu daima yatakuwa ya msingi na ya maana pindi hayo mateso  yakitokana na utumishi wa kumtumikia Mungu. Yeyote yule ambaye anateseka kwa ajili ya kumtumikia Mungu akiiga mfano wa yule mwanakondoo, kwake huyo twaweza sema na bainisha kuwa anaishi yale mateso halisi ya Kristu msulubiwa. Hivyo daima tukumbuke kuwa siyo kila shida, mateso/ mahangaiko katika maisha twaweza yalinganisha na yale ya Kristu. Yule ambaye amejisababishia shida, mateso kwa uzembe au kwa sababu ya kutenda dhambi hatuwezi sema kuwa hayo ni mateso shirikishi katika yale mateso ya mwanakondoo wa Mungu. Mateso shirikishi katika yale mateso ya mwanakondoo wa Mungu, ni yale mateso ambayo tunayashiriki kwa ajili ya kuwa wafuasi kamili ya huyo mwanakondoo wa Mungu.


Tuna picha ya huyo mwanakondoo wa Mungu ambaye daima yeye daima huwa siyo mwenye kulipa visasi na kutumia nguvu dhidi ya maadui wake. Hii imedhihirishwa katika kitabu cha nabii Isaia 53:7 " Alionewa, lakini yeye alinyenyekea, wala hakufunua kinywa chake; kama mwanakondoo apelekwaye machinjioni, na kama vile kondoo anyamazavyo mbele yao wakatao manyoya yake; Naam hakufunua kinywa chake." Hivyo ni dhahiri kuwa hii picha ya mwanakondoo inatutafakarisha kuwa daima amani huwa hailetwi kwa nguvu au suruba au kulipiza visasi, bali huletwa kwa fadhila ya unyenyekevu na msamaha.


Tunapata picha pia ya mwana-kondoo wa Mungu kuwa ni mtumishi asiye tafuta faida mbele ya wengine ( suffering servant) daima basi tutambue kuwa tunavyomtumikia Mungu, tusitangulize faida au maslahi mbele kwani huyo Mungu aliyetuita tumtumikie ndiye ajuaye namna na jinsi ya kuwalisha na kuwatunza wale ambao amewaita wamtumikie. Daima hapa tunapata changamoto juu ya swala zima la uchungaji na wachungaji wetu, kuwa daima hawa wachungaji kipau mbele cha kwanza katika kumtumikia Mungu kwao nini? ni maslahi binafsi au ni kumtumikia Mungu bila ya kuangalia hayo maslahi? hapo ni jukumu letu kujitafakari na kuiga huo mfano wa mtumishi asiyetafuta faida au maslahi binafsi.


Tusisahau pia kuwa hii picha ya mwana-kondoo kwetu sisi inagusia dhana ya ushindi. Basi kumbe huyu mwanakondoo anayeongelewa ni anatupa habari njema ya ushindi. Kitabu cha ufunuo kinabainisha huo ushindi ambapo inaelezwa kuwa, " wakisema kwa sauti kuu, Astahili Mwana-Kondoo aliyechinjwa, kuupokea uweza na utajiri na hekima na nguvu na heshima na utukufu na baraka." ( ufunuo5:12), " hawa watafanya vita na mwana-kondoo, na Mwana kondoo atawashinda, kwa maana yeye ni Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme, na hao walio pamoja naye ndio walioitwa, na wateule, na waaminifu.( ufunuo17:14) hivyo twaweza tambua kuwa huyo mwana-kondoo tunayeelezewa habari habari zake kwa unyenyekevu wake anajitwalia mamlaka, uweza na ushindi.

Ni kwa msingi huu twaweza baini kuwa wakati wa ibada ya misa takatifu hasa tukifika kile kipengere cha mwanakondoo wa Mungu( Agnus Dei), huwa tunaimba utenzi wa mwanakondoo au kama siyo kuimba huwa tunatamka maneno yake. na wakati huo kuhani huwa anachukua kipande cha mkate ulio altareni na kukivunja. Juu ya hilo tendo Mtakatifu Yohane Chrisostom ( 407) alikuwa na haya ya kusema, " Kwa kile ambacho Kristu hakukitesekea msalabani, anateseka kwa hii sadaka ya ekaristi takatifu kwa ajili yenu." Hayo maneno huwa tunasikia daima padre akiyarudia daima na daima pale ashikapo mwili wa Yesu na kusema maneno yafuatayo, " huyu ndiye mwana-kondoo wa Mungu aondoaye dhambi za dunia heri yao walioalikwa kwenye karamu ya Bwana..." Hivyo tunavyoadhimisha ibada ya misa takatifu daima tunamwangalia yule mwana-kondoo aliyeteseka, akafa, na akafufuka kwa ajili ya wokovu wetu. Daima yatupasa kuizunguka meza ya Bwana kwa moyo wenye toba na unyenyekevu tukimwomba tuwe watumishi wake na tumtumikie.



No comments:

Post a Comment