Tuesday, 31 January 2017

MAHUBIRI YA JUMAPILI YA TANO KIPINDI CHA KAWAIDA MWAKA A.


1. Isa 58: 7-10
2.1Kor2:1-5
Injili:Mt5:13-16

               " Tunaitwa kuwa chumvi na mwanga kwa dunia."

Wapendwa taifa la Mungu leo tunaadhimisha jumapili ya tano ya kipindi cha mwaka wa Kanisa. Katika kusheherekea jumapili hii, wazo muhimu na wazo kuu litakalotuongoza katika ibada yetu, ni kuwa sote kama wabatizwa wana wa Mungu tunaalikwa kuwa ' chumvi na mwanga kwa dunia'.

Masomo yetu ya leo hasa somo la injili linagusia maisha yetu katika ujumla wake hasa somo linagusia sisi kuwa kielelezo na mfano kwa wale ambao bado hawana maisha na fadhila za kikristu. Jumapili iliyopita tulisikia juu ya heri nane ambazo zilikuwa taratibu kwa yeyote yule kuingia katika ufalme wa mbinguni. Leo hii tunafundishwa juu ya kuwa mwanga na chumvi kwa ulimwengu ili tupate kuwavuta wengine na kuwafanya wakutane na Kristu.

Bwana wetu Yesu Kristu anatumia mfano wa chumvi na mwanga. Hii ni mifano halisi inayokubalika moja baada ya nyingine kadiri tunavyofahamu matumizi ya chumvi na mwanga. Kama chumvi ikiachwa bila kutumiwa kwenye chakula, hiyo chumvi haitokuwa na maana ya matumizi yake. Kama taa ipo lakini haiwezi ikaangaza mahala palipo giza ili watu wapate kuona vizuri, hiyo taa pia haitokuwa na maana kamwe. Chumvi pale inapowekwa kwenye chakula hutambulika uwepo wake maana hiyo chumvi huwa kikolezo cha radha katika chakula. Taa pia itatambulika umuhimu wake pindi ikiwashwa na kuwaangazia watu ili wapate kuona vyema.

Katika tafakari yangu basi nitatafakari nanyi nyote juu ya zile sifa kuu muhimu za chumvi nikizilinganisha na maisha yetu wakristu.

Kwanza, chumvi ikiwekwa kwenye chakula huwa inafanya chakula kinakuwa na radha ya aina yake. Kwa wale tutumiao chumvi katika chakula tunafahamu ni kwa jinsi gani na namna gani chakula hupoteza radha na hata hupoteza hamu kwa mlaji pindi ikikosekana chumvi. Vivyo hivyo kwetu sisi wakristu tunawajibu wa kuwa chumvi ( mifano bora kwa wengine) kadiri ya maisha yetu. Maisha yetu ni ushuhuda wa Kristu kwa wale ambao hawajampokea Kristu. Maneno yetu, mawazo yetu, matendo yetu hivyo vyote ni vielelezo ambavyo vyaweza kuwavuta wengine kwa Kristu Yesu. Maisha yetu ni injili inayomhubiri Kristu hata kwa wale wenzetu ambao siyo wakristu. Mawazo, maneno, na matendo yangu, ni karamu moja nzuri ya kuandika ujumbe wa Kristu katika maisha na mioyo ya wengine. Tukikaa wakristu jina hatutokosa kufananishwa na ile chumvi ambayo ipo ila haitumiki.

Pili, chumvi hufanya kazi ya kutunza chakula kisiharibike. Kabla ya kuja uvumbuzi wa vifaa vya umeme vyenye kuhifadhi vyakula visiharibike ( fridge) zamani mababu na mabibi zetu, japo hata leo hii njia yawezekana bado ikawa bado ipo, walitumia chumvi katika kuhifadhia chakula chao, kama vile nyama na vyakula vingine vingi ambavyo viliweza kuhifadhiwa kwa muda mrefu kwa kutumia chumvi. Kwa upande wetu wetu wakristu tunakumbushwa na huo mfano kuwa ni kwa jinsi gani twaweza tunza tunu na fadhila zetu za kikristu siku zote za maisha yetu. Maisha ya ufuasi wa Kristu yana maana kubwa pindi zile tunu na fadhila zake zikiwa kama kielelezo na ngao yetu na utambulisho wetu katika maisha yetu kama wafuasi wake Kristu.

Tatu, chumvi huleta kiu. Twaweza jiuliza kitu kimoja kuwa ni mara ngapi maisha yetu kama wakristu yamekuwa ni chachu ya kuleta kiu kwa wengine ili wawe wafuasi pia wa Kristu? kwa maneno yake Kristu mwenyewe anabainisha: " Ninyi ni nuru kwa mataifa,"( Mt5:14). Katika dunia yetu leo ninini kinatokea na ninini kinaendelea? daima tunajikuta hatuna au hatutoi picha picha nzuri kwa ulimwengu kufuatana na mawazo, maneno na matendo yetu sisi wenyewe kutoendana na mafundisho ya Bwana wetu Yesu Kristu. Kuna mtu mmoja ambaye amewahi kuwa maarufu duniani aliwahi sema haya maneno: " Ninampenda Yesu Kristu, ila siupendi ukristu," kuwa mafundisho ya Kristu ni mazuri sana yenye tunu na fadhila nzuri, ila sisi waumini tunapata changamoto moja kubwa kuwa zile tunu nzuri na fadhila za kikristu zinabaki vitabuni au kwenye maandishi tu bila ya kushuka ardhini.

Katika mikutano mbalimbali ya madhehebu ya wajiitao walokole daima tunapata changamoto kubwa sana tena sana kutoka kwa hao wainjilishaji wa Kilokole kwa kuwa wao daima humhubiri yule Yesu mtoa adhabu kali kwa yule asiyemwamini Yesu kuwa ni Bwana na mwokozi! Binafsi sijui kama hii iko sawa au hapana. Labda nitaikubali hii tu pale ambapo watahubiri kwa kutoleta mashambulizi kwa madhehebu mengine au kwa kuwashambulia wengine kwa kuhubiri kwa mifano bora ya kuigwa kuliko kuhubiri kwa misimamo hasi peke yake.


Katika maisha yetu sisi kama wafuasi wa kristu bado tunakumbana na changamoto kubwa sana hasa kwa upande wa wachungaji ( watawa, mapadre, na maaskofu). Huwa ninini daima kinatokea pindi kuhani akianguka katika majaribu na dhambi? tumepata kushuhudia kuwa wapo makuhani ambao kwa madhaifu yao wameshindwa kulinda utu na heshima yao, wengi wameshuhudiwa tayari wakiwa ni walevi, na wengine kwa kuoa na kuzaa watoto na kutelekeza ile kazi waliyoitiwa na Bwana, hilo ni jambo ambalo katika uwazi na ukweli lipo na limekwisha kutokea. 


Changamoto kwetu sisi waumini tukiona hayo yanatokea kwa wale ambao wamewekwa tuwe chini yao huwa tunafanya nini? daima kitu ambacho huwa kinatokea kusambaza hayo matendo ya makuhani yasiyopendeza kwa wengine ikiwezekana hata kwa njia ya mitandao ya kijamii, kama vile whatsapp, facebook, youtube, twitter, n.k. Lakini kwa kuuliza swali moja tu la msingi ni kwamba, ni nani kati yenu aliwahi chukua muda wake akaaa chini na kuwafikiria hao wachungaji/ makuhani na akaamua kuwaweka kwenye sala na maombi ili basi roho mtakatifu azidi kutawala zaidi katika maisha yao na hatimaye wabadili mitizamo na mienendo yao?? ni mara ngapi waumini tumechukua nafasi kukaa karibu na hao wachungaji wetu na kuwa kitulizo kwao hasa kutokana na magumu wanayoyapitia kama binadamu wengine? kama ukikumbuka kuwaombea hao wachungaji wako basi wewe ni mwenye bahati, maana pia hao mapadre wako na maaskofu wako wanataka kusikia mazuri na kujifunza kutoka kwako wewe muumini, maana kila mmoja ameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu ili awe chumvi na mwanga kwa mwingine.

Thursday, 26 January 2017

MAHUBIRI YA JUMAPILI YA NNE YA MWAKA A KIPINDI CHA KAWAIDA.


1.Zefania 2:3;3:12-13
2.1Kor 1:26-31
Injili: Mt5:1-12

             

                    " Njia itupelekayo kwenye raha ya milele"


Wapendwa taifa la Mungu niwakaribishe katika tafakari ya masomo yetu ya jumapili ya nne ya kipindi cha kawaida cha mwaka wa Kanisa mwaka A. Neno linalotuongoza leo katika tafakari yetu ni, ' ni njia ipi hasa inatupatia raha ya milele katika maisha yetu?" Kitu ambacho hutuangaisha sisi binadamu hapa duniani daima huwa ni kutafuta chochote ambacho hutufanya tuwe na raha na hatimaye kufurahi' au tuseme daima binadamu huangaika hapa na pale ili mwisho wa siku apate raha au aweze kustarehe, hilo ni jambo ambalo kila mmoja wetu hulitafuta kwa gharama yoyote ile. "Hata hivyo tatizo ni kwamba kile watu wakifikiricho kuwa kitawaletea raha daima katika maisha, kimsingi huwa hicho hakileti raha ya kweli" ( Aristotle).


Hebu chukulia mfano wa yule mtu anayeamini kuwa akinunua chupa ya bia, au chupa ya whisky akainywa kwake anafikiria kuwa hiyo inamletea raha. Huyo mtu  akinywa chupa ya bia au whisky na akaendesha gari lake kurudi nyumbani kwa sababu ya ulevi au kutojitambua anaendesha hilo gari hovyo bila kwa kusahau kuwa kuna alama za barabarani, na matokeo yake huyo huishia kuparamia nguzo za umeme, au kuparamia makorongo na kuumia vibaya kesho yake mtu huyo hujikuta akiwa hospital kwa chumba cha watu waliokaribu kukata roho, huku mikono na miguu yake vimefungiwa bandage n.k hivyo ni kwa msingi huo hatuwezi kusema kuwa vitu vya namna hiyo na vinginevyo vyaweza tuletea raha daima katika maisha, ila hivyo huleta raha za muda, raha zenye kupita kuliko ile raha ya milele.


Leo tunapoadhimisha jumapili ya nne ya mwaka wa Kanisa tunakumbushwa juu ya raha ya milele jinsi tunavyoweza kuipata. Mwinjili Matayo katika injili anagusia zile njia za kuipata raha ya milele, nazo si nyingine bali ni zile heri nane. Daima kama unasafiri pale mahali usipopajua huwa ni vyema kutembea na ramani ndogo mkononi ili ikupe maelezo halisi ya pale uendapo. Katika Injili ( Mt 5:1-12) Yesu anatupa ramani ya kutembea nayo ili hiyo ramani iweze kutufikisha pale raha ya milele ilipo ( ufalma we mbinguni).


Yesu anapoanza utume wake anaanza kwa kusisitiza kuhusu hizi heri nane, sasa tujiulize kuwa kwa nini aweke msisitizo katika hizo heri nane? ni kwa sababu ya umuhimu wa hili fundisho. Kama nilivyoisha elezea hapo awali, ni kwamba kila mmojawetu hapa duniani huweka juhudi ili mwisho wake apate furaha. Ukifanywa utafiti kwa watu mbalimbali juu ya nini kiwafanyacho kuwa na furaha yatapatikana majibu mbalimbali, na yale majibu yakijaribu kulinganishwa na yale majibu Yesu anayotufundisha katika injili leo, twaweza baini kuwa yatakuwa majibu tofauti.
Pale Yesu asemapo, " Heri waliomaskini wa roho" "watu husema heri yao walio matajiri." Pale Yesu asemapo, " heri wenye uzuni"," watu husema heri yao wale wenye utani." Pale Yesu asemapo, "heri wenye huruma," watu baadala yake husema, " heri wenye nguvu na hasira." pale Yesu "asemapo heri wenye upole," watu hesema, " heri yao wale walio maridadi na wenye nguvu." Pale Yesu asemapo "heri wenye njaa na kiu ya haki," watu husema, " heri yao wenye mvinyo wa kutosha mezani kwa ajili ya kusindikiza mlo." Pale Yesu asemapo, " heri wenye moyo safi," watu baadala yake husema, " heri yao waliobarikiwa kuwa na vitambi na ngozi laini." Pale Yesu asemapo " heri yao wapatanishi," watu husema, " heri yao watengeneza habari." Pale Yesu asemapo, " heri yao wadharauliwao na kushutumiwa" watu baadala yake husema, " heri yao wale ambao wana mawakili wazuri wa kuwatetea."


Twaweza baini na tambua kabisa kuwa mafundisho ya Bwana wetu Yesu Kristu juu ya hizo heri nane, ambazo kimsingi ndoo ramani ituoneshayo njia ya kwenda mbinguni kimsingi zipo kinyume kabisa na utamaduni wa ulimwengu katika ujumla wake. Kwa kuziishi hizo heri nane ni kama kupingana na utamaduni ulimwengu. Ni kwamba haiwezekani tukakubali mafundisho ya Kristu halafu upande mwingine tukakumbatia utamaduni dunia, tunaalikwa tuchukue kimojawapo na tuache kimojawapo,tuchukue kimojawapo ambacho ni cha msingi kwetu, ambacho ndoo kinatupeleka katika ile furaha na raha ya milele.


Tutambue kuwa Yesu katika mafundisho yake kwetu juu ya hizi heri nane hamaanishi kuwa tuachane na yale tuyafanyayo, yale yanayotuwezesha kuishi, bali fundisho lake kwetu sote ni kwamba kwa yale yote tuyafanyayo tumtangulize Mungu mbele kwanza, tutumie yale yote tuliyonayo kama nyenzo ya kutufikisha kwa Mungu baadala ya kutuangamiza. Mfano, kama unamiliki simu ya gharama, basi tumia hiyo fursa ya kumiliki simu ya gharama kuwainjilisha watu, kuwaletea watu habari njema, kurahisha mawasiliano muhimu, kuliko kuitumia hiyo simu ya ghrama kufanya yasiyopendeza machoni pa Mungu, kama una utajiri wa pesa, basi tumia hizo pesa kwa kuwasaidia wale wasiojiweza baadala ya kutumia hizo pesa kwa mambo yasiyo ya lazima na msingi, kama umejaliwa na akili nyingi, tumia hiyo akili yako nyingi kuwahelimisha watu, kufanya uvumbuzi kwa ajili ya kuleta maendeleo baadala ya kutumia hiyo akili kufanya uvumbuzi wenye kuleta maangamizi kwa wengine. Kama umejaliwa kipaji tumia hicho kipaji kwa ajili ya kumtukuza Mungu baadala ya kutumia hicho kipaji kujitukuza mbele ya wengine. Kama umejaliwa kupenda nguo, basi penda nguo ambazo ukizivaa hazileti aibu kwa wengine, nk. Ni kwa msingi huo ni lazima yale tuliyo nayo tuyatumie katika kuhakikisha kuwa yanatufikisha mahali ambapo kuna raha ya milele.


Hizo heri nane tulizozisikia katika Injili siyo kuwa hizo heri zinalenga watu wa aina nane duniani ambapo tweweza weka maswali na kujiuliza daima kuwa mimi/fulani anaangukia katika kundi lipi la hizo heri nane, hapana hizi heri nane ni mwaliko kwa kila mmoja wetu kujitafakari na kubadilika kwa kuelekea kwa Kristu zaidi. Swali la motisha kwetu ni kwamba maisha yetu huwa yanazamia upande gani zaidi? katika kumwelekea Kristu au duniani zaidi? Kwa kuishi mafundisho ya Kristu ni uhakika wa kuipata ile raha ya milele.



Saturday, 21 January 2017

MAHUBIRI JUMAPILI YA TATU YA MWAKA A KIPINDI CHA KAWAIDA


1. Isa 9:1-4
2.1Kor 1:10-13,17
Injili: Mt 4:12-23

            " Ili kupata samaki wazuri uvumilivu wahitajika"

Wapendwa katika Kristu, leo tunaadhimisha jumapili ya tatu ya kipindi cha kawaida cha mwaka ambapo katika masomo yetu hasa somo la Injili tunasikia Yesu anawaita wafuasi wake wa kwanza kabisa:  Peter, Andrea, Yakobo na Yohane ( Mt4:12-23). Hawa walioitwa kumfuata Kristu kazi yao kabla ya hapo ilikuwa ni kuvua samaki, lakini tunaona leo Yesu anawaita wawe wafuasi wake ili wawe ni wavuvi wa watu. Hawa ni kundi la watu ambao walikuwa na mtizamo na fikra za aina fulani katika maisha yao, lakini Kristu anatumia hiyo fursa ya huo mtizamo wao kuwa fursa yenye mtizamo zaidi ya ule mtizamo waliokuwa nao wale wavuvi wa samaki, huo mtizamo wa Bwana wetu Yesu Kristu kwa wale aliowaita wawe wafuasi na wanafunzi wake, ni mtizamo wa kutoka na kuingia ndani zaidi kwenye maisha ya watu baadala ya maisha ya viumbe vingine.


Ndugu wapendwa katika Kristu tunapata kujifunza kuwa Kristu anvyowaita hawa wafuasi wake wa kwanza kuacha kazi ya uvuvi na kumfuata ili wawe wavuvi wa watu, tunapata fundisho kuwa ziwa/ bahari daima kadiri ya tafsri ya maandiko matakatifu ni ishara ya uovu/ubaya, hivyo Kristu anavyowaambia kuwa waende duniani wakawavue watu, anagusia dhana ya watu waovu, na maovu yao duniani. Dunia tunayoishi imejaa mema na maovu pia, hii dunia yaweza pia chukua picha/taswira ya ziwa au bahari ambapo ziwani au baharini kuna aina mbalimbali za viumbe, wakiwemo samaki wa aina mbalimbali. Ni katika mtizamo huu tunaona Yesu anawaita hawa waende katika ile bahari kubwa sana ili waweze kuwavua watu, kwa maana ya kuwafundisha watu fadhila za Krikristu kutoka fadhila za kidunia.


Swali ambalo twaweza jiuliza na pia likapata kutuongoza katika tafakari yetu ni kwamba kwa nini Yesu anawaita hawa wavuvi? twaweza jibu hili swali tukiambatanisha sifa alizo nazo mvua samaki. Kwa msingi huu hizi ndoo sifa ambazo anazo mvua samaki Kristu anazitumia katika kutufikishia ujumbe wa Neno la Mungu. Hebu tuone hizo sifa:


Kwanza, mvua samaki ni mtu ambaye ana uvumilivu wa hali ya juu. Daima mvua samaki huwa na uvumilivu katika kufanya kazi yake ya kuvua akirusha ndoana au jalife bahari au ziwani au mtoni huwa anakuwa na subira hadi kuhakikisha kuwa samaki wanaingia katika hilo jalife. Ni kwa msingi huu twaweza baini kuwa katika kuwahubiri Neno la Mungu wale ambao bado hawajaipata habari njema ya wokovu, daima kunahitaji uvumilivu, maana watu hawawezi wakabadilishwa na mahubiri au tafakari ya siku moja, hivyo ni lazima na muhimu kuwa na uvumilivu katika kutangaza habari njema ya Bwana. Walisikialo neno la Bwana hupata kuelewa Neno, na kubadilika kufuatana na uvumilivu wa mchungaji.


Pili, mvua samaki daima huwa na ile sifa ya kutokata tamaa. Daima mvuvi akirusha ndoana baharini, hasipofanikiwa hurudia tena na tena hadi kuhakikisha kuwa anafanikiwa, hivyo kwetu ni fundisho kuwa katika maisha yetu ya Kikristu hatuhitaji kukata tamaa pale ambapo tunaona maisha yetu ya utume, maisha yetu kama wakristu hayaendi, au pale ambapo tunaona giza katika maisha ya ufuasi wa Bwana wetu  Yesu Kristu, daima kwa neema ya Mungu tunahitaji tuwe imara na tuwe na ile roho ya kutokata tamaa.


Tatu, mvua samaki huwa na ile sifa ya kuwa shupavu. Mvua samaki daima huwa yupo tayari kukumbana na mawimbi makali ya bahari au ziwa au mto, huwa tayari kuweka maisha yake mdomoni mwa wanyama wakali wa bahari kama vile Mamba, Nyangumi, viboko, nk hayo yote huyapitia ili aweze kupata anachohitaji kupata katika safari yake. Vile vile wahubiri, wachungaji daima hupata changamoto katika bahari ya maisha. Daima huwa ni changamoto kuwahubiria watu ukweli na wote wakaukubali ukweli. Hivyo daima ni dhahiri kuwa katika kuhubiri ukweli lazima yule atangazaye Neno la Mungu hupata changamoto za kutukanwa, au kukataliwa kwa sababu ya kusimamia ukweli wa Neno la Mungu. Yule ahubiriye ukweli ndoo yule atakaye chukiwa na ndugu zake, atakayetemewa mate na saa nyingine atakeye tukanwa na watu, yule asimamaye katika njia ya haki na ukweli daima huwa na marafiki wachache. Katika hili tunaalikwa kuuishi kuhubiri na kuishi ukweli.


Nne, mvuvi daima huwa ana akili ya kusoma alama za nyakati katika kutenda kazi yake.  Mvua samaki hujua kuwa haya ni majira ya kupata samaki wengi, na pengine hujua na kutabiri kuwa muda fulani siyo rahisi kuwapata samaki. Anajua ni lini arushe jarife baharini, au aweke ndoana baharini. Mvuvi anajua tosha kuwa siyo kila majira samaki wana patikana kwa wingi, bali yeye hujua majira ya kuwapata samaki wengi na majira ambapo samaki huwa daima ni wachache au saa nyingine hakuna kabisa. Hivyo katika kutangaza Neno la Bwana hatuna budi kusoma alama za nyakati na kutambua kuwa huu ni wakati wa watu kuukubali ujumbe wa Neno la Mungu, au hu ni wakati watu kutokubali kiurahisi Neno la Mungu. Ni kwa msingi huu twaweza baini muda wa kusikiliza{ kutafakri} na muda wa kuongea na watu.


Tano, mvuvi mwerevu huwa na anajua namna ya kutupa chambo baharini au ziwani ili apate kumpata samaki vyema. Mhubiri mzuri ni yule anayetambua kuwa hawezi  kuwavuta watu wote kwake, mtangaza Neno la Mungu, daima anahitaji kujua mazuri yake na mapungufu yake. Hivyo katika kutangaza Neno la Bwana daima tutambue kuwa kuna nyakati ambazo kile tukihubilicho kinaendana na maisha yetu wenyewe, na pia maisha ya watu tuwahubilio.


Mwisho, mvuvi mwerevu daima huwa anajitahidi kuficha kivuli chake pindi avuapo samaki, maana hasipoficha hicho kivuli hatofanikiwa kupata hata samaki mmoja. Vivyo hivyo muhubir mzuri na mwerevu hawahubiri au hatangazi Neno la Bwana kufuatana na hisia na vionjo vyake, bali muhubiri mwema na mzuri  huwahubiria watu maisha Kristu. Mhubiri mwema daima huvaa utu na sura Kristu. Mhubiri ni Kristu mwingine katika kuwafanya watu walielewe neno la Mungu. Lengo la mhubiri daima ni kuwafanya watu waweke macho na mioyo yao kwa Kristu kuliko kuwafanya watu wahamishie mioyo na macho yao kwake ( kuishi maisha yenye kupendeza, maisha yenye kumbeba na kumpeleka Kristu kwa wengine).


Ndugu wapendendwa twaweza tambua kuwa kila mmoja wetu ameitwa na Bwana katika kumtumikia, hivyo ni mwaliko kwetu sote kutumia kalama zetu, na mapaji yetu tuliyojaliwa na Mungu katika kuhubiri Neno la Bwana. Kila mmoja anaitwa na Kristu na kutumwa na Kristu kuwa mmisionary pale alipo. Lile lolote ambalo kila mmoja wetu afanyalo alifanye kwa utukufu wa Bwana kwani ni huyo Bwana ambaye hutoa kwa kila mmoja wetu kadiri ya mapenzi yake.


                                                                                                      

Wednesday, 11 January 2017

MAHUBIRI JUMAPILI YA PILI YA MWAKA A


Isa 49:3; 5-6
2.1Kor 1:1-3
Injili:1:29-34

                    " Je na wewe ni mwanakondoo?"

Wapendwa familia ya Mungu tunaposheherekea jumapili ya pili ya kipindi cha kawaida cha mwaka wa Kanisa tunaalikwa kutafakari juu ya Yesu kama mwanakondoo wa Mungu. Wazo kuu ambalo litatuongoza katika tafakari yetu ni juu ya huyo mwanakondoo wa Mungu kwetu ana maana gani na je twaweza kujifunza nini kutoka kwake huyo mwana kondoo wa Mungu.

Katika Injili tunamsikia mwinjili Yohane akigusia hili jambo kwa ukaribu, katika Injili Yohane anasema, " tazama mwanakondoo wa Mungu aondoaye dhambi za dunia"( Yohane1:29). Katika mazingira ya kawaida na uelewa wetu wa kawaida pindi tusikiapo neno, " Mwanakondoo"  picha ambayo hutujia akilini mwetu ni juu ya yule mtu ambaye ni mpole sana, mnyenyekevu, au yule ambaye hana sauti katika jamii. Lakini hata hivyo tunapata motisha hapa kuwa Yesu alikuwa hana hiyo picha ya mwanakondoo kama wengi ambavyo tunaweza fikiria. Baadala yake Yesu ni mwanakondoo ambaye amepewa sifa ya kuondoa dhambi za dunia, hivyo huyo ni mwanakondoo mwenye nguvu, ni mwanakondoo hasiye dhaifu, ni mwanakondoo ambaye yupo tayari kuufia ukweli. Huyu ni mwanakondoo ambaye yupo tayari kubeba  hata lawama ili atimize mapenzi ya Mungu.

Kutoka katika maandiko matakatifu twaweza pata picha mbili juu ya huyo mwanakondoo. Kwanza kabisa ni kuwa huyo mwanakondoo damu yake inamwagika kwa ajili ya wengine. Hii taswira ya huyo mwanakondoo ambayo mwinjili Yohane anatufundisha katika injili inapata mizizi yake kutoka moja ya vitabu vya agano la kale. " Nao watatwaa baadhi ya damu yake na kuitia katika miimo miwili na katika kizingiti cha juu katika zile nyumba watakazomla."( Kut12:7) "

Kwa kuwa Bwana atapita ili awapige hao wamisri; na hapo atakapoiona hiyo damu katika kizingiti cha juu, na katika ile miimo miwili, Bwana atapita juu ya mlango, wala hatamwacha mwenye kuharibu aingie nyumbani mwenu."( Kut 12: 23). Ni kwa msingi huo tunapata ufahamu na uelewa juu ya hii taswira ya Yesu kama mwanakondoo kuwa Yeye ajitoa sadaka kwa ajili ya wengine. Ni kwa msingi huu twaweza sema juu ya utumishi, kuwa yeyote ambaye anataka kuwa kiongozi lazima auvae ule utu wa Kristu kama mwanakondoo. Yeyote ambaye ni kiongozi kwa maana ya kuwatumikia watu, huyo hana budi kuitwa mwanakondoo. Kuwa kiongozi katika hii taswira/picha ya mwanakondoo ni kukubali kukabiliana na hali zote yakiwemo magumu katika kumfuasa Kristu mwanakondoo wa Mungu. 


Mateso katika maisha yetu daima yatakuwa ya msingi na ya maana pindi hayo mateso  yakitokana na utumishi wa kumtumikia Mungu. Yeyote yule ambaye anateseka kwa ajili ya kumtumikia Mungu akiiga mfano wa yule mwanakondoo, kwake huyo twaweza sema na bainisha kuwa anaishi yale mateso halisi ya Kristu msulubiwa. Hivyo daima tukumbuke kuwa siyo kila shida, mateso/ mahangaiko katika maisha twaweza yalinganisha na yale ya Kristu. Yule ambaye amejisababishia shida, mateso kwa uzembe au kwa sababu ya kutenda dhambi hatuwezi sema kuwa hayo ni mateso shirikishi katika yale mateso ya mwanakondoo wa Mungu. Mateso shirikishi katika yale mateso ya mwanakondoo wa Mungu, ni yale mateso ambayo tunayashiriki kwa ajili ya kuwa wafuasi kamili ya huyo mwanakondoo wa Mungu.


Tuna picha ya huyo mwanakondoo wa Mungu ambaye daima yeye daima huwa siyo mwenye kulipa visasi na kutumia nguvu dhidi ya maadui wake. Hii imedhihirishwa katika kitabu cha nabii Isaia 53:7 " Alionewa, lakini yeye alinyenyekea, wala hakufunua kinywa chake; kama mwanakondoo apelekwaye machinjioni, na kama vile kondoo anyamazavyo mbele yao wakatao manyoya yake; Naam hakufunua kinywa chake." Hivyo ni dhahiri kuwa hii picha ya mwanakondoo inatutafakarisha kuwa daima amani huwa hailetwi kwa nguvu au suruba au kulipiza visasi, bali huletwa kwa fadhila ya unyenyekevu na msamaha.


Tunapata picha pia ya mwana-kondoo wa Mungu kuwa ni mtumishi asiye tafuta faida mbele ya wengine ( suffering servant) daima basi tutambue kuwa tunavyomtumikia Mungu, tusitangulize faida au maslahi mbele kwani huyo Mungu aliyetuita tumtumikie ndiye ajuaye namna na jinsi ya kuwalisha na kuwatunza wale ambao amewaita wamtumikie. Daima hapa tunapata changamoto juu ya swala zima la uchungaji na wachungaji wetu, kuwa daima hawa wachungaji kipau mbele cha kwanza katika kumtumikia Mungu kwao nini? ni maslahi binafsi au ni kumtumikia Mungu bila ya kuangalia hayo maslahi? hapo ni jukumu letu kujitafakari na kuiga huo mfano wa mtumishi asiyetafuta faida au maslahi binafsi.


Tusisahau pia kuwa hii picha ya mwana-kondoo kwetu sisi inagusia dhana ya ushindi. Basi kumbe huyu mwanakondoo anayeongelewa ni anatupa habari njema ya ushindi. Kitabu cha ufunuo kinabainisha huo ushindi ambapo inaelezwa kuwa, " wakisema kwa sauti kuu, Astahili Mwana-Kondoo aliyechinjwa, kuupokea uweza na utajiri na hekima na nguvu na heshima na utukufu na baraka." ( ufunuo5:12), " hawa watafanya vita na mwana-kondoo, na Mwana kondoo atawashinda, kwa maana yeye ni Bwana wa Mabwana, na Mfalme wa Wafalme, na hao walio pamoja naye ndio walioitwa, na wateule, na waaminifu.( ufunuo17:14) hivyo twaweza tambua kuwa huyo mwana-kondoo tunayeelezewa habari habari zake kwa unyenyekevu wake anajitwalia mamlaka, uweza na ushindi.

Ni kwa msingi huu twaweza baini kuwa wakati wa ibada ya misa takatifu hasa tukifika kile kipengere cha mwanakondoo wa Mungu( Agnus Dei), huwa tunaimba utenzi wa mwanakondoo au kama siyo kuimba huwa tunatamka maneno yake. na wakati huo kuhani huwa anachukua kipande cha mkate ulio altareni na kukivunja. Juu ya hilo tendo Mtakatifu Yohane Chrisostom ( 407) alikuwa na haya ya kusema, " Kwa kile ambacho Kristu hakukitesekea msalabani, anateseka kwa hii sadaka ya ekaristi takatifu kwa ajili yenu." Hayo maneno huwa tunasikia daima padre akiyarudia daima na daima pale ashikapo mwili wa Yesu na kusema maneno yafuatayo, " huyu ndiye mwana-kondoo wa Mungu aondoaye dhambi za dunia heri yao walioalikwa kwenye karamu ya Bwana..." Hivyo tunavyoadhimisha ibada ya misa takatifu daima tunamwangalia yule mwana-kondoo aliyeteseka, akafa, na akafufuka kwa ajili ya wokovu wetu. Daima yatupasa kuizunguka meza ya Bwana kwa moyo wenye toba na unyenyekevu tukimwomba tuwe watumishi wake na tumtumikie.



Friday, 6 January 2017

MAHUBIRI YA JUMAPILI YA UBATIZO WA BWANA WETU YESU KRISTU


1. Isa42: 1-4,6-7
2. Mdo 10:34-38
Injili: Mt 3:13-17

"  Daima tufanywe viumbe wapya katika Kristo kwa njia ya ubatizo wetu"


Kuna kisa cha mtu mmoja aliyeenda kwa muuza nguo na mshona nguo, aliingia mahali pale na kuangaza kuzunguka katika hilo duka la muuza nguo kwa kuangalia mavazi mbalimbali yaliyokuwemo mle dukani, na baadaye huyo mtu ambaye umri wake kidogo ulikuwa ni umri wa uzee alirudi kwa huyo muuza nguo na kumwambia, tafadhali naomba unitengezee vazi zuri la kike namna ya mkaja lakini lisiwe kubwa liwe dogo kiasi, maana kesho ni siku ya mjukuu wangu. Huyo mtu aliendelea kubainisha kuwa lile vazi lilikuwa kwa ajili ya mjukuu wake.


Mtengeneza nguo alipata kuwa na shahuku ya kujua umri wa huyo aliyekuwa akiombewa na Babu yake atengenezewe hiyo nguo maalum, " mjukuu wako ana miaka mingapi?", mzee alijibu," hadi sasa ninapoongea hii ni siku ya saba tangia azaliwe" mtengeneza nguo alibaki ameduwaa kwa kuwa hilo lilikuwa siyo jambo la kawaida. Hivyo huyo mzee aliendelea kusisitiza hilo vazi litengenezwe vizuri kwa kusema, " hakikisha hilo vazi linapendeza, maan kesho ni siku ambapo mjukuu wangu ni siku yake yakukutana na Mungu" kwa mshangao yule muuza nguo aliendelea kuwa na wasiwasi, kwa kumuuliza tena yule mzee kwa mshangao," kukutana na na Mungu?? mzee alijibu, " kesho ni siku yake ya kubatizwa"


Wengi wetu hata kama siyo wote tulibatizwa tukiwa bado wadogo sana kiasi kwamba saa nyingine huwa inatuwia vigumu kukumbuka ile siku muhimu katika maisha yetu ambapo tulibatizwa na tukawa wana wa Mungu. Hatuwezi kukumbuka na kujua ni namna gani siku ya ubatizo wetu wazazi wetu, wazazi wetu wa ubatizo walivyokuwa wanajibu maswali na kukiri imani kwa niaba yetu?? Huu ndoo wakati ambapo tulipata majina yetu kwa njia ya ubatizo.


Leo ni siku ambayo tunafanya sherehe ya ubatizo wa Bwana wetu Yesu Kristu, twaweza jiuliza maswali mengi sana juu ya kwanini Yesu alipata kubatizwa kule mto Yordani?  Sakramenti ya ubatizo maana yake huwa ni kuondoa dhambi ya asili, hivyo twaweza jiuliza kuwa hivi Yesu alibatizwa kwa kuwa alikuwa na dhambi ya asili pia? Jibu ni kwamba hakuwa na hiyo dhambi ya asili, na kwa kubainisha hilo mtakatifu Ambrozi mwalimu wa Kanisa alikuwa na haya ya kusema juu ya ubatizo wa Bwana wetu Yesu Kristu:  " Bwana wetu Yesu Kristu alibatizwa si kwa sababu ya dhambi ya asili, bali alibatizwa ili akayasafishe na kuyatakasa maji ili yawe
na nguvu ya ubatizo" 


Ni kwa msingi huo tunaona Kristu anabatizwa ili apate kuunganika na sisi katika ubinadamu wetu uliodhaifu hasa akiungana nasi katika ile safari yetu ya hija ya ufalme wa mbinguni. Hivyo yupo nasi na ni mmoja wetu. Kila mmoja wetu atambue amezaliwa na dhambi ya asili, Kanisa ni chombo cha Mungu ambapo hiyo dhambi ya asili huondolewa na hivyo sisi kuitwa watoto wa Mungu. Naye mtakatifu Vincent Ferrer alikuwa na haya ya kusema juu ya ubatizo; " kila mkristu mbatizwa inabidi atambue kuwa ni ndani ya tumbo la Kanisa kila mmoja wetu hugeuzwa kutoka kuwa mwana wa Adamu kuwa mwana wa Mungu."dhambi ya adamu iliyofanya wote tukawa na dhambi ya asili, hiyo dhambi ya asili huondolewa na nguvu ya sakramenti ya ubatizo na hivyo kutufanya tusiwe chini ya uvuli wa Adamu, bali tuwe viumbe wapya katika Kristu.


Ubatizo kwetu maana yake ninini?ubatizo ni sakramenti tuipokeayo, ambayo hutuosha dhambi ya asili na hatimaye sisi huitwa wana wa Mungu. Daima ili tuwe wana wa Mungu ni lazima sote tushiriki ule ubatizo wa Bwana wetu Yesu Kristu. Kristu anavyobatizwa ni kiashilio cha kuanza kwa utume wake, ni kiashilio cha kutangaza ufalme wa mbinguni hapa duniani, wengine waliozoea lugha ya wanasiasa utasikia hapa na pale wanasema neno, ' sela' na vivyo hivyo kwa ubatizo Kristu mwenyewe anajiweka wakfu kwa ajili ya kazi aliyotumwa kufanya duniani, na kazi kubwa kuliko zote ilikuwa ni kuutangaza ufalme wa Mungu kwa mataifa na vizazi vyote.


Kwa njia ya ubatizo tunazaliwa upya kwa maji na Roho Mtakatifu. Tunakuwa tumetakaswa kutoka dhambi ya asili na hivyo tunakuwa wana wa Mungu. Kwa njia ya ubatizo huwa ndo tunaingizwa Kanisani na kuwa moja ya jamii ya wakristu wanaounda kanisa duniani. Hii hatua ya kuingizwa kanisani kwa waliobatizwa yaweza fananishwa na moja ya mila zetu ambapo mmojawapo akitaka kuhesabiwa kuwa ni mmoja wa wanaukoo fulani katika jamii husika, hupitia hatua iitwayo jando( initiation- rites of passages) sasa nasi wakatoliki tuko sambamba na lile lifanyikalo katika tamaduni zetu, sisi jando yetu huwa ni kumwandaa mtoto/mkatekumeni kwa hatua ili aweze kupokelewa kanisani na hatimaye kuwa mwanajumuiya kamili wa kanisa linaloungama imani moja.

Sakramenti ya ubatizo ni alama na ishara inayotukumbusha kuwa tumejiweka wakfu katika ufalme wa Mungu. Kupitia ubatizo ni dhahiri kuwa huwa tunakuwa tayari kumtumikia Mungu kama manabii, wafalme, na makuhani. Kwa njia ya sakramenti ya ubatizo huwa tunaimarishwa pia na roho mtakatifu, kwani ile siku ambayo kila mmoja wetu hubatizwa humpokea roho mtakatifu pia. Huyo roho mtakatifu tumpokeaye wakati wa ubatizo ni yule roho ambaye hutupa nguvu za kupambana na vishawishi na pia kupambana na magumu mbalimbali.

Juu ya nguvu ya Sakaramenti ya ubatizo Papa Benedict xvi alikuwa na haya ya kusema, " thamani ya ubatizo  ni msingi imara wa umissionari kwa kila mmoja wetu aliyebatizwa, kwa kuwa yule ambaye amependa kumshuhudia Kristo Yesu kwa njia ya ubatizo ni lazima afuate nyayo zake yule aliyemshuhudia kwa njia ya matendo. Hivyo kwa njia ya ubatizo tumekuwa warithi katika kufanya kazi ya Bwana kwa njia ya umissionari."


Kwa kumalizia hebu tuangalie zile sifa kuu za Kristu aliyebatizwa, je naweza kulinganisha hizo sifa za Yesu mbatizwa na maisha yangu?
Yesu alikuwa maskini lakini mimi siyo maskini.
Yesu alikuwa mnyenyekevu na mtii, lakini mimi siyo mtii.
Yesu alikuwa mpole, lakini mimi siyo mpole.
Yesu alisamehe, lakini mimi naweka roho ya kulipiza visasi.
Yesu alitii mamlaka, lakini mimi daima hutaka kutotii na saa nyingine kuwaamlisha wengine kwa faida yangu.
Yesu alichukiwa kwa sababu ya ukweli, mimi nauzika ukweli ili nipendwe zaidi na nilinde maslahi yangu.
Yesu alipaa mbinguni kwa njia ya mateso na msalaba, lakini mimi kwa upande wangu nataka kufika huko kwa njia ya starehe na raha bila ya msalaba.

Je hiyo ni sawa kuwa mtumishi awe hivyo kuliko yule mwalimu wake?

Thursday, 5 January 2017

MAHUBIRI YA JUMAPILI YA EPIFANIA MWAKA A


1. Isa.60: 1-6
2.Ef 3:2-3,5-6
Injili: Mt 2:1-12

"  Hata asili yaweza kuongea na kumpeleka mtu kwa Mungu"

Ndugu zangu basi niwaalike tuweze kutafakari Neno la Mungu pindi tunapoadhimisha Jumapili ya tokeo la Bwana wetu Yesu Kristu yaani, Epifania.

Katika masomo yetu hasa somo la injili twaweza baini kuwa katika safari yetu ya imani kuna aina tatu za watu; wale ambao humtafuta Mungu na kumtumikia; wale ambao wanamtafuta Mungu lakini bado hawajamwona; na mwisho wale ambao hawana haja/shauku ya kumtafuta Mungu. Kundi la kwanza la aina ya watu wamtafutao Mungu ni lile kundi la watu wenye amani na furaha, kundi la pili ni lile kundi la watu wenye uso wa huzuni kwa sababu wanamtafuta Mungu lakini hawajamwona katika maisha yao, nalo kundi la tatu ni kundi la wajinga, yaani wale ambao hawana hata hamu ya kukutana na Mungu mwumba wao.

Tunaona hizo aina tatu za wale wamtafutao Mungu kama inavyodhihirishwa katika masomo yetu, hebu tuone aina mojawapo, ambayo hii ni aina ya tatu ya wale wamtafutao Mungu, yaani kundi la wajinga ambao hawa daima hujifanya wanamtafuta Mungu kumbe ndani yake wana hila ya kufanya maovu kwa kutumia hiyo nafasi. Basi ni kwa msingi huu twaweza sema kuwa aina hii ya tatu kadiri ya somo la injili inaangukia kwa mfalme Herode, huyu anajifanya kumtafuta Mungu kumbe anazo hila nyingi ndani yake, yeye lengo lake ilikuwa kutafuta kumwua Yesu ili apate kulinda madaraka yake yasipokonywe na huyo mfalme aliyezaliwa. Tunaambiwa kuwa mfalme Herode kwa kusutwa na dhamila yake mbaya anaamua kuwa ua hata watu wa familia yake akiwemo mke wake Mariamme na watoto wake wawili. Herode kimsingi anawakilisha kundi la watu ambao hutumia madaraka vibaya, watu ambao hujifanya wako karibu na Mungu kumbe wana malengo mengine.

Pia tunaona kundi jingine la wale wamtafutao Mungu na kukutana naye na hatimaye kumtumikia, basi hili siyo kundi jingine bali ni Yosefu na Maria, na pia katika hilo kundi twaweza kujumuisha wale wachungaji( Lk2:8-12). Hivyo ni kwa msingi huu twaweza sema kuwa hili ni kundi lenye amani na furaha kwa kuwa wamekumkutana na Mungu.


Kundi jingine la watu wamtafutao Mungu, ni Mamajusi, hawa ni wale wamtafutao Mungu kwa nguvu zao zote na juhudi zao zote bila ya kuchoka. Mamajusi ni neno ambalo lina msingi wake kutoka lugha ya Kigiriki " Magoi" ambapo nalo hilo limezaa neno la kiingereza, " magic" au " magician" hawa mamajusi walikuwa siyo wachawi kama tuwaonao kwenye mazingira yetu, bali hawa walikuwa ni wataalamu wa nyota, na hivyo katika ufumbuzi wao walikuwa wakitaka kujua uhusiano uliopo kati ya nyota na dunia. Hawa kwa ujuzi na utaalamu wao waliitwa watu wa hekima kwa kuwa wao walifuata alama za asili na hizo alama za asili ziliwaongoza hadi kwa Kristu.


Kwa upande wetu ni nyota ipi ambayo inaweza tupeleka kwa Kristu? Je mimi ni nyota ya kumpeleka mwingine kwa Kristu? Ni nyota ipi ya kwanza ambayo ilikupeleka wewe kwa Kristu Yesu?? Jibu ni kwamba ile nyota ya kwanza ambayo ilinipeleka mimi na ikakupeleka kwa Kristu Yesu ni wazazi wetu/ walezi wetu pindi tulivyokuwa wadogo au tukishakuwa watu wazima, tukiikumbuka ile siku yetu ya kwanza tulipobatizwa na kuitwa wana wa Mungu katika Yesu Kristu mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote. Wazazi wetu/ au walezi wetu, au malezi mazuri ya Kikristu na elimu ya maandiko matakatifu, walimu na watu wenye maarifa mbalimbali, kwa msingi huo twaweza sema kuwa,  hizo zote ni nyota ambazo zimetupeleka kwa Kristu na hizo ndoo nyota ambazo zinatuongoza hadi kwa Kristu hadi leo hii.


Mamajusi walimpelekea Yesu dhahabu, uvumba, na manemane,zikiwa ni alama za mali asili za dunia. Hata hivyo kwa upande wetu sisi hatuna haja ya kumpelekea Mungu dhahabu, manemane, na uvumba, baadala yake sisi Yesu tunampelekea Mioyo yetu, akili zetu na utashi wetu wa kumtumikia na kukaa naye daima, hizo kimsingi ndoo zawadi zetu kubwa kwa Yesu Kristu. Dhahabu, uvumba na manemane vyaonekana kuwa vilikuwa ni vitu vya thamani sasa kwa wakati ule hata hadi nyakati zetu.


Hawa mamajusi kwa kubeba hivyo vitu na kumpelekea Kristu ni fundisho kwetu kuwa hawa, wanatupa ishara ya kuacha mali dunia, kuacha mambo mengi ya dunia yenye thamani na kisha kumtafuta Kristu na hatimaye kuweza kukaa naye. Sisi upande wetu nasi twaweza labda jiuliza swali moja kubwa kuwa ni vingapi tulivyo navyo kama vile utajiri, hela na mali nyinginezo zinatuzuia kwenda kwa Kristu? hawa mamajusi wametumia huo utajiri ili uweze kuwafikisha kwa Kristu.


Kumbe kwetu nasi hili liwe somo na fundisho kuwa vile vyote tulivyonavyo kama mali, utajiri na vingine vingi, basi kumbe twaweza vitumia kama njia ya kutufikisha kwa Yesu Kristu. Mfano kama unamiliki gari, basi hilo gari litumie liwasaidie watu baadala ya kuleta matatizo, kama una miliki simu ya kisasa, tumia hiyo nafasi ya kumiliki hiyo simu katika kuinjilisha na kumtangaza Kristu baadala ya kutumia hiyo simu kutenda maovu, kama una akili nyingi, basi itumie hiyo akili uwasaidie watu wapate kumfikia Kristu kwa urahisi, kama wewe ni daktari basi tumia hicho kipaji cha utabibu ili uwape watu maisha baadala ya kuwaondolea maisha, kama wewe ni mwalimu, basi wafundishe watu mambo mazuri na njia njema za kufika kwa Kristu, na kama wewe ni padre, askofu, mchungaji, basi tumia hiyo kalama yako ya huo uchungaji ili uwavute watu kwa Kristu Yesu.  Ni kwa msingi huo mimi naweza sema kuwa pia ni mamajusi na wewe ni mamajusi wa kupeleka tulichonacho kwa Kristu na kubaki naye daima.


Nimalizie tafakari hii kwa kisa hiki: Kulikuwa na mtu mmoja ambaye alifanya kazi katika kiwanda cha pamba, huyu alikuwa ni mkristu aliyejiwekea utaratibu wa kutokula nyama siku za ijumaa akiendelea kutafakari mateso ya Kristu msalabani. Huyu daima siku za ijumaa alibeba mayai na samaki kidogo kwa ajili ya mlo wake pindi awapo kazini. Hivyo wafanyakazi wenzake ambao walikuwa siyo wakatoliki walimtania na kumbatiza jina la " Bwana mayai na masamaki" wakati wao siku zote walikuwa wakila wali kwa nyama. Na mbali ya kutaniwa na kufanyiwa kejeli za namna hiyo, huyo ndugu hakuacha ule utaratibu wake wa kubeba hicho kitoweo chake siku za ijumaa.


Huyo mtu miaka baadaye alipata kukutana na mtu mmoja ambaye alikuwa amevalia mavazi ya upadre akitokea Kanisani, hao wawili walipata kutambuana na hivyo kupata kuhabarishana mambo mengi sana.


Hapo baadaye  huyo padre aliyekuwa akitoka mlango wa Kanisa alimwambia yule ndugu: " Ilikuwa ni mfano wako mzuri ndoo ulinifanya niingie ukatoliki. Nilikumbuka zile siku ambazo ulikuwa unabeba samaki na mayai kazini kwako na pia ukaanza kudhalauliwa na kuchekwa na ndugu zako uliofanya nao kazi, lakini na mbali ya hayo madharau hukuacha/ kuikana imani yako, na umedumu kwa kuilinda imani yako, nami kwa kuona hivyo nikaamua kujiunga na ukatoliki maana nilifikiri sana kuwa kama huyu amedharauliwa namna hiyo na akazidi kuishi na kuilinda imani yake, vivyo ni lazima kutakuwa na kitu cha pekee kwa wakatoliki. Ni kwa jinsi hiyo niliamua kufuata imani ya Kanisa Katoliki. Leo nimeadhimisha misa yangu ya kwanza ya Shukurani." huyo padre alimalizia kutoa ushuhuda wake kwa huyo ndugu.


Epifania maana yake ni kumdhihirisha Kristu, kumfunua Kristu kwa wale ambao bado hawajapata kutambua uwepo wake katika maisha yao. Kwa kuwainjilisha watu kwa mifano bora hasa kupitia maisha yetu tunavyoishi, ni dhahiri kuwa sisi tunakuwa ni nyota za kuwapeleka watu kwa Kristu.


Tutabaki kujiuliza hili swali kuwa je mimi ni nyota ya kuwapeleka watu kwa Kristu? Je kama ni nyota nimewapeleka wangapi kwa Kristu? Daima tuwe nyota zenye mwanga wa kuwapeleka watu kwa Kristu.