Thursday, 26 January 2017

MAHUBIRI YA JUMAPILI YA NNE YA MWAKA A KIPINDI CHA KAWAIDA.


1.Zefania 2:3;3:12-13
2.1Kor 1:26-31
Injili: Mt5:1-12

             

                    " Njia itupelekayo kwenye raha ya milele"


Wapendwa taifa la Mungu niwakaribishe katika tafakari ya masomo yetu ya jumapili ya nne ya kipindi cha kawaida cha mwaka wa Kanisa mwaka A. Neno linalotuongoza leo katika tafakari yetu ni, ' ni njia ipi hasa inatupatia raha ya milele katika maisha yetu?" Kitu ambacho hutuangaisha sisi binadamu hapa duniani daima huwa ni kutafuta chochote ambacho hutufanya tuwe na raha na hatimaye kufurahi' au tuseme daima binadamu huangaika hapa na pale ili mwisho wa siku apate raha au aweze kustarehe, hilo ni jambo ambalo kila mmoja wetu hulitafuta kwa gharama yoyote ile. "Hata hivyo tatizo ni kwamba kile watu wakifikiricho kuwa kitawaletea raha daima katika maisha, kimsingi huwa hicho hakileti raha ya kweli" ( Aristotle).


Hebu chukulia mfano wa yule mtu anayeamini kuwa akinunua chupa ya bia, au chupa ya whisky akainywa kwake anafikiria kuwa hiyo inamletea raha. Huyo mtu  akinywa chupa ya bia au whisky na akaendesha gari lake kurudi nyumbani kwa sababu ya ulevi au kutojitambua anaendesha hilo gari hovyo bila kwa kusahau kuwa kuna alama za barabarani, na matokeo yake huyo huishia kuparamia nguzo za umeme, au kuparamia makorongo na kuumia vibaya kesho yake mtu huyo hujikuta akiwa hospital kwa chumba cha watu waliokaribu kukata roho, huku mikono na miguu yake vimefungiwa bandage n.k hivyo ni kwa msingi huo hatuwezi kusema kuwa vitu vya namna hiyo na vinginevyo vyaweza tuletea raha daima katika maisha, ila hivyo huleta raha za muda, raha zenye kupita kuliko ile raha ya milele.


Leo tunapoadhimisha jumapili ya nne ya mwaka wa Kanisa tunakumbushwa juu ya raha ya milele jinsi tunavyoweza kuipata. Mwinjili Matayo katika injili anagusia zile njia za kuipata raha ya milele, nazo si nyingine bali ni zile heri nane. Daima kama unasafiri pale mahali usipopajua huwa ni vyema kutembea na ramani ndogo mkononi ili ikupe maelezo halisi ya pale uendapo. Katika Injili ( Mt 5:1-12) Yesu anatupa ramani ya kutembea nayo ili hiyo ramani iweze kutufikisha pale raha ya milele ilipo ( ufalma we mbinguni).


Yesu anapoanza utume wake anaanza kwa kusisitiza kuhusu hizi heri nane, sasa tujiulize kuwa kwa nini aweke msisitizo katika hizo heri nane? ni kwa sababu ya umuhimu wa hili fundisho. Kama nilivyoisha elezea hapo awali, ni kwamba kila mmojawetu hapa duniani huweka juhudi ili mwisho wake apate furaha. Ukifanywa utafiti kwa watu mbalimbali juu ya nini kiwafanyacho kuwa na furaha yatapatikana majibu mbalimbali, na yale majibu yakijaribu kulinganishwa na yale majibu Yesu anayotufundisha katika injili leo, twaweza baini kuwa yatakuwa majibu tofauti.
Pale Yesu asemapo, " Heri waliomaskini wa roho" "watu husema heri yao walio matajiri." Pale Yesu asemapo, " heri wenye uzuni"," watu husema heri yao wale wenye utani." Pale Yesu asemapo, "heri wenye huruma," watu baadala yake husema, " heri wenye nguvu na hasira." pale Yesu "asemapo heri wenye upole," watu hesema, " heri yao wale walio maridadi na wenye nguvu." Pale Yesu asemapo "heri wenye njaa na kiu ya haki," watu husema, " heri yao wenye mvinyo wa kutosha mezani kwa ajili ya kusindikiza mlo." Pale Yesu asemapo, " heri wenye moyo safi," watu baadala yake husema, " heri yao waliobarikiwa kuwa na vitambi na ngozi laini." Pale Yesu asemapo " heri yao wapatanishi," watu husema, " heri yao watengeneza habari." Pale Yesu asemapo, " heri yao wadharauliwao na kushutumiwa" watu baadala yake husema, " heri yao wale ambao wana mawakili wazuri wa kuwatetea."


Twaweza baini na tambua kabisa kuwa mafundisho ya Bwana wetu Yesu Kristu juu ya hizo heri nane, ambazo kimsingi ndoo ramani ituoneshayo njia ya kwenda mbinguni kimsingi zipo kinyume kabisa na utamaduni wa ulimwengu katika ujumla wake. Kwa kuziishi hizo heri nane ni kama kupingana na utamaduni ulimwengu. Ni kwamba haiwezekani tukakubali mafundisho ya Kristu halafu upande mwingine tukakumbatia utamaduni dunia, tunaalikwa tuchukue kimojawapo na tuache kimojawapo,tuchukue kimojawapo ambacho ni cha msingi kwetu, ambacho ndoo kinatupeleka katika ile furaha na raha ya milele.


Tutambue kuwa Yesu katika mafundisho yake kwetu juu ya hizi heri nane hamaanishi kuwa tuachane na yale tuyafanyayo, yale yanayotuwezesha kuishi, bali fundisho lake kwetu sote ni kwamba kwa yale yote tuyafanyayo tumtangulize Mungu mbele kwanza, tutumie yale yote tuliyonayo kama nyenzo ya kutufikisha kwa Mungu baadala ya kutuangamiza. Mfano, kama unamiliki simu ya gharama, basi tumia hiyo fursa ya kumiliki simu ya gharama kuwainjilisha watu, kuwaletea watu habari njema, kurahisha mawasiliano muhimu, kuliko kuitumia hiyo simu ya ghrama kufanya yasiyopendeza machoni pa Mungu, kama una utajiri wa pesa, basi tumia hizo pesa kwa kuwasaidia wale wasiojiweza baadala ya kutumia hizo pesa kwa mambo yasiyo ya lazima na msingi, kama umejaliwa na akili nyingi, tumia hiyo akili yako nyingi kuwahelimisha watu, kufanya uvumbuzi kwa ajili ya kuleta maendeleo baadala ya kutumia hiyo akili kufanya uvumbuzi wenye kuleta maangamizi kwa wengine. Kama umejaliwa kipaji tumia hicho kipaji kwa ajili ya kumtukuza Mungu baadala ya kutumia hicho kipaji kujitukuza mbele ya wengine. Kama umejaliwa kupenda nguo, basi penda nguo ambazo ukizivaa hazileti aibu kwa wengine, nk. Ni kwa msingi huo ni lazima yale tuliyo nayo tuyatumie katika kuhakikisha kuwa yanatufikisha mahali ambapo kuna raha ya milele.


Hizo heri nane tulizozisikia katika Injili siyo kuwa hizo heri zinalenga watu wa aina nane duniani ambapo tweweza weka maswali na kujiuliza daima kuwa mimi/fulani anaangukia katika kundi lipi la hizo heri nane, hapana hizi heri nane ni mwaliko kwa kila mmoja wetu kujitafakari na kubadilika kwa kuelekea kwa Kristu zaidi. Swali la motisha kwetu ni kwamba maisha yetu huwa yanazamia upande gani zaidi? katika kumwelekea Kristu au duniani zaidi? Kwa kuishi mafundisho ya Kristu ni uhakika wa kuipata ile raha ya milele.



No comments:

Post a Comment