Friday, 3 February 2017

MAHUBIRI JUMAPILI YA 6 MWAKA A KIPINDI CHA KAWAIDA


1. Ybs :15:15-20
2.1Kor 2:6-10
Injili: Mt 5:17-37

           " Kuchagua siyo shida, bali shida ninini unachagua"

Katika moja ya hadithi ambazo nimewahi zisoma, na hii ni mojawapo: Ilitokea wadhambi wawili walimwendea padre ili wapate kuungama, walipofika kwa padre walikuwa na haya ya kumwambia, " Baba padre tumefika hapa na tuko mbele yako, sisi ni wakosefu, hivyo twahitaji msaada wako wa  sakramenti ya kitubio." Mmoja kati ya wale wadhambi alimwambia padre kuwa yeye dhambi zake ni kubwa, na mwingine akamwambia padre kuwa dhambi zake ni ndogondogo kiasi kwamba hajisikii kuziungama. Baada ya hayo maongezi padre aliwaomba wote wawili walete mawe, kila mmoja alete mawe kadiri ya dhambi zao walizotenda. Mmoja alienda akaleta jiwe moja kubwa sana, na mwingine akaleta mawe mengi madogomadogo kwenye mfuko. Basi baada ya kupeleka hayo mawe kwa yule padre, padre aliwaamuru pia kurudisha hayo mawe kila moja katika nafasi lilipotoka jiwe. Yule aliyekuwa ameleta jiwe kubwa alijitahidi kuliviringisha kadiri ya uwezo wake na kulirudisha mahala pake, na yule mwingine aliyekuwa ameleta mawe madogomadogo kwenye mfuko, alianza kusumbuka na kubabaika huku akikosa la kufanya, na baadaye alimwambia padre kuwa ilikuwa ni vigumu kwake kuweza kukumbuka nafasi ya kila jiwe alipolitoa maana yalikuwa ni mawe madogo sana kiasi kwamba alisahau hata nafasi za yale mawe yalipokuwa. Baadaye yule padre aliweza kuwapa maana ya kile alichowaambia wakafanye. Padre alisema kuwa, yule aliyeleta jiwe kubwa maana yake ni kwamba alikuwa na dhambi kubwa sana ambapo ilichukua nafasi kubwa katika moyo wake, hivyo kwa kuishi na hiyo dhambi hakukumpa raha kamwe bali daima alikaa akikumbuka kuwa lazima akaungame hiyo dhambi na kutubu, na kwa yule aliyeokota mawe madogo madogo pia padre alimwambia kuwa hayo mawe madogomadogo ni kielelezo cha dhambi ndogondogo ambazo mbele ya fikra na macho ya binadamu huonekana kuwa hazina umuhimu wa kuziungama na hivyo kuweza kusahulika kiurahisi sana. Hivyo huyo padre alimalizia kwa kuwaambia kuwa wote wanahitaji kuungama na hatimaye kupata huruma ya Mungu mbali ya kuwa na dhambi kubwa na ndogo. Padre alimalizia kwa kusema kuwa dhambi ni dhambi na sakramenti ya kitubio ndoo yahitajika kuiondoa hiyo dhambi.

Wapendwa katika masomo yetu ya leo, katika injili tunapata habari njema ya Bwana wetu Yesu Kristu, hasa juu ya ile hotuba aliyotoa mlimani akiwa na wafuasi wake. Hotuba hii wengine huichukulia kama muhtasari wa mafundisho yake Bwana wetu Yesu Kristu. Tumeanza kuisikia hiyo hotuba pale juu ya zile heri nane. Leo katika injili ya mtakatifu Mathayo5:17-37, tunaambiwa namna dhambi itendwavyo, dhamira ya kutenda dhambi, madhara na upotofu wa maadili utokanao na dhamira ya kutenda dhambi.


Katika injili tunafundishwa kuwa dhambi hutendwa kuanzia katika fikra iwapo mtu analengo la kutenda uovu hata kama hatofanikiwa kuhalalisha uovu huo kimatendo basi hiyo inahesabika kama dhambi, hata isipotendwa, kwa kuwa kinachoangaliwa hapa ni dhamira au nia ya mtu. Mfano yawezekana mtu mmoja akawa na chuki na mtu mwingine kiasi cha kudhamiria hata kumwondoa uhai, kadiri ya injili huo tayari ni uuaji maana dhamira tayari ilikuwepo, hii ni sawasawa na uzinzi, maana kitendo cha kutamani mwanamke au mwanaume tayari huo ni uzinifu ndani ya roho ya yule atamaniye. Ni kwa msingi huu huwa daima katika ile sala ya nakuungamia Mungu mwenyezi katika ibada takatifu ya misa huwa tunasema, " ..........nanyi ndugu zangu kwani nimekosa muno kwa mawazo, kwa maneno, na kwa matendo..... hivyo hiyo ni dhahiri kuwa dhambi yaweza tendwa katika hizo hali.


Katika Biblia tunasoma kuwa, "kwa maana ndani ya mioyo ya watu hutoka mawazo mabaya, uasherati, wivi, uuaji, uzinzi, tamaa mbaya, ukorofi, hila, ufisadi, kijicho, matukano, kiburi, upumbavu. Haya yote yaliyo maovu yatoka ndani, nayo yamtia mtu unajisi"(Mk7:21-23). Tunafundishwa kutoka katika Biblia kuwa moyo wa binadamu ni chanzo cha yale yote ayatendayo binadamu, ndani ya moyo wa mwanadamu yamejificha mengi sana. Ni katika msingi huo tunaalikwa kuchagua yale yaliyo mema na kuacha yale mabaya, tunaalikwa kuiga yale yaliyomema kutoka kwa wengine na siyo kuyaiga yale yaliyo mabaya kwao. Katika kitabu cha Yoshua bin Sira tunaambiwa juu ya hayo pia kuwa, " ukipenda utazishika amri zake na kutenda amini ni shauri lako. Ameweka mbele yako moto na maji utanyosha mkono wako uchaguavyo." Ybs15:15-16.


Dhambi maana yake ninini? tunaambiwa kuwa dhambi ni matokeo ya kufanya kinyume na mapenzi yake Mungu muumba wetu. Tukiendelea mbele zaidi twaweza sema kuwa dhambi ni pale ambapo binadamu hukataa kuupoke ule upendo wa Mungu usio na kikomo. Kuna mwandishi fulani wa vitabu aliyepata kusema kuwa kuna aina 700 za dhambi ambazo hata hivyo zaweza kuwekwa kwenye makundi makuu matatu. Kundi la kwanza la dhambi ni ile dhambi ya kutotii mamlaka ya Mungu. Mfano juu ya hili ni ile dhambi ya Adamu na Hawa. Mungu aliwambia wasile tunda la mti wa kati, lakini wao kwa kiburi chao wakakahidi hilo agizo."( Mwanzo 2: 15-17). Hii dhambi hata nyakati zetu bado inaendelea kujidhihirisha. Huwa daima katika maisha tunajikuta katika hali ambapo mmoja hupata kusema mimi najua kila kitu, mimi ni mwanzo wa maarifa yote hivyo sihitaji kumsikiliza fulani au kufundishwa na fulani. Lakini tunaalikwa daima kuwa watii kwa mamlaka, kwani mamlaka hupata uweza na nguvu kutoka kwa Mungu.

Pili ni dhambi kati ya ndugu kwa ndugu. Katika maandiko matakatifu tunapata kisa cha Kaini kumwua ndugu yake Abel ( Mw4:8) katika hiki kisa chenye kuhudhunisha tunaona kuwa Kaini anaamua kumtoa uhai ndugu yake kwa sababu ya chuki na wivu. Kwa moyo wenye chuki, masengenyo na wivu katika maisha ya mkristu, huo moyo yabidi usafishwe kwa sakramenti ya kitubio, kwani kumchukia mtu na kumdhamilia vibaya huko ni kumwua.

Tatu, dhambi ya kuwa na kiburi. Tunapata habari ya kisa cha kujengwa mnara wa Babel katika kitabu cha agano la kale katika Biblia. ( Mw11:1-9). Kisa au historia hii inatuelezea jinsi watu walivyokuwa wakaidi wakaamua kujenga mnara mrefu ili wafike pale Mungu alipo. Huu mnara ni kilelezo cha mwanadamu kujitukuza, mwanadamu kujiona anauwezo kama wa Mungu, mwanadamu kujifanya Mungu mbele ya wanadamu wenzake, mwanadamu kujiona kuwa pasipoyeye mambo hayawezekani, na mwanadamu kupenda kukaa juu ya wengine na kuwatawala pasipo ridhaa yao. Hao wajenga mnara hawakuweza kumfikia Mungu kwa kuwa wao kwa wao hawakuweza kusikilizana, kuwa na lugha moja na kauli moja. Vivyo hivyo katika maisha yetu daima hatuwezi kumwona Mungu na kujua alipo pindi sisi wenyewe tukikosa kuwa wamoja na pia kuwa na lugha moja ya kutuunganisha kama watoto wake. Daima kiburi ni sumu kubwa katika mahusiano,kwani hakuna hata mmoja ambaye daima hudiliki kusemezana na wenye majivuno. Kiburi daima huaribu urafiki kati ya watu. Daima upendo wa Kristu hauwezi tawala maishani mwa kila mmoja wetu, pindi lugha ya mimi, baadala ya sisi, ninyi, na wao isipotawala katika maisha yetu.

Ndugu wapendwa daima sote tunaalikwa kuwa wafuasi bora wa Kristu na siyo bora wafuasi. Daima tunaalikwa kuiga mifano yake Bwana wetu Yesu Kristu. Kama yeye alitimiza mapenzi yake Baba wa mbinguni kwa kufa msalabani basi nasi kwetu ni mwaliko kuishi upendo wa namna hiyo hata kuwa tayari kutoa uhai wetu kwa ajili ya wengine.